|

SHERIA ZA FUNGA NA ADABU ZAKE
Baada ya kumshukuru Allah
Subhana Wataala na kumsalia Mjumbe wake Sayyidna Muhammad s.a.w. pamoja na
sahaba zake na kila anayefuata njia yake
Umma wa
Kiislamu:
Tambueni ya
kwamba (taqwa) uchamungu una cheo kikubwa katika dini ya kiislamu , na
wachamungu wana daraja za juu kwa mujibu wa maelezo ya qur-ani, kwa hivyo
wachamungu ndiyo vipenzi vya Allah:
إن أولياؤه إلاّ المتّقون .
Hawakuwa walinzi wake isipokuwa wachamungu tu .
Na
wachamungu ndiyo vipenzi vya Allah:
والله وليّ المتّقين .
Na Allah ni rafiki wa wale wamchao .
Na kwa hivyo watafuzu
kukubwa mno siku ya kiama:
والآخرة عند ربّك للمتّقين .
Na akhera iliyo kwa mola ni ya wenye kumcha Allah .
Na ilivyokuwa funga ni
njia imfikishayo mtu katika uchamungu , basi huwa ni wajibu kwa muislamu
kuitekeleza vile ipasavyo , na ajitahidi kikomo cha uwezo wake katika
kufuata adabu zake na kutochupa mipaka yake , ili funga yake imfikishe
katika daraja za wachamungu na imuepushe na moto na kumtia katika pepo ,
anasema Allah Mtukufu:
فمن
زحزح عن النار وأدخل الجنة فقد فاز ، وما الحياة الدنيا إلا متاع الغرور .
Na aliyewekwa mbali na
moto na akaingizwa peponi , basi amefuzu . Na maisha ya dunia hii si kitu
ila ni starehe idanganyayo .
Ndugu Waislamu:
Hakika
funga inayofungwa na waislamu wengi siku hizi , sio hiyo funga inayotakiwa
hasa kisheria , kwa sababu funga zao hazizidi zaidi ya kujizuwia na kula
na kunywa na huupitisha mchana wao kwa uvivu na kutojishughulisha na kazi
yoyote , mpaka linapokuchwa jua huanza kuvamia vyakula vya kila namna
kisha hukesha usiku wake katika starehe na mchezo , basi mtu wa namna hii
hutoka katika ramadhani kama alivyoingia , hakupata maghfira wala
hakuufikia uchamungu .
Kwa hivyo
ni vyema tutambue kuwa funga ambayo amewaamrisha Allah waja wake kuifunga
, na ikawa ndiyo njia imfikishayo mtu katika uchamungu na kumuepusha na
moto , ina adabu zake na mipaka yake na ina shuruti na ahkamu zake , kwa
hivyo funga ni kujizuwiya na yale yote yenye kufunguza katika wakati wake
maalumu , pamoja na kujuwa ulifanyalo na kutia nia . Na miongoni mwa
sheria za funga ni kujizuwiya na kuingiza kitu chochote katika tundu ya
mwili ifikishayo ndani ya tumbo , ikiwa kitu hicho ni chakula au si
chakula , na inakatazwa kutoa kitu ndani ya tumbo kwa makusudi kama
kujitapisha , na anatakiwa mtu anapokuwa ndani ya funga , ajizuwiye na
maingiliano baina yake na mkewe au kujitowa manii kwa makusudi .
Na ikiwa
kitaingiya kitu tumboni bila ya kukusudia , basi huwa hapana kitu kwa
aliyefunga kwa mfano makohozi ikiwa hayakufika mdomoni bali yamepita kooni
, ama yakifika mdomoni basi ni lazima ayateme na inakatazwa kukusanya mate
kisha kuyameza na kwa aliyetapika bila ya kukusudia huwa hapana neno
isipokuwa asikimeze kile kilichobaki mdomoni , imekuja katika hadithi
kutoka kwa Mtume s.a.w. amesema:
من ذرعه القيء فليس عليه قضاء ، ومن استقاء فليقض .
Aliyetapika bila ya
kukusudia huwa hapana kitu , na kwa aliyejitapisha kwa makusudi basi alipe
.
Na aliyefunga anatakiwa
wakati wa kutia udhu asipeleke sana maji katika pua .
Na inampasa kwa aliyefunga
kujiepusha na kila linaloamsha matamanio , kwa sababu kujitoa manii kwa
makusudi kunaharibu funga , na kwa aliyepatwa na janaba mchana wa
ramadhani akimbilie kuoga , na kwa aliyelala na mkewe anatakiwa kuoga
kabla ya kupambazukiwa na alfajiri kama ilivyokuja katika hadithi sahihi
isemayo :
من أصبح جنبا أصبح مفطرا .
Atakayepambazukiwa hali
ya kuwa na janaba huwa amepambazukiwa akiwa hana funga .
Ndugu Waislamu:
Kwa hakika kuna jambo
linamfunguza aliyefunga ambalo wengi wetu tumeghafilika nalo , na huharibu
funga za watu kama alivyosema Mtume s.a.w. :
ربّ صائم حظّه من صيامه الجوع والعطش ، وربّ قائم حظّه من
قيامه السّهر .
Huwenda kwa aliyefunga
ikawa sehemu yake ni kukaa na njaa na kiu na huwenda kwa anayesimama kwa
ajili ya kusali ikawa sehemu yake ni kukesha tu.
Kwa hivyo maasi na makosa
hubatilisha funga anasema Mtume s.a.w.:
لا صوم إلا بالكف عن محارم الله .
Hapana funga ila kwa
kujizuwiya na makatazo ya Allah .
Na amesema vilevile :
من
لم يدع قول
الزور والعمل به فليس لله حاجة أن يدع طعامه وشرابه .
Asiyewacha kusema uongo na
vitendo vyake basi Allah hana haja ya mtu kuwacha chakula na kinywaji
chake .
Na yametajwa baadhi ya
madhambi yavunjayo funga kwa mfano :
الغيبة تفطّر الصائم وتنقض الوضوء .
Kusengenya kunamfunguza
aliyefunga na kunaharibu udhu .
Na anatakiwa anayefunga
ajiepushe na kulipa uovu aliotendewa imekuja katika hadithi :
فإذا كان يوم صوم أحدكم فلا يرفث ولا يصخب ، فإن سابّه أحد أو
قاتله فليقل إنّي صائم .
Anapokuwa mmoja wenu
katika funga asitukane wala asigombane , na akitukanwa au akitakiwa
kupigana basi aseme mimi nimefunga .
Kwa hivyo hadithi hizi na
nyenginezo ni dalili ya kwamba maasi yanaharibu funga na kupoteza ujira
wake na humzuwia mtu kuufikia uchamungu .
Na funga ina wakati wake
uliowekwa na sheria , huanza kwa kuchomoza alfajiri ya kweli na humalizika
kwa kukuchwa jua , anasema Allah
وكلوا واشربوا حتّى يتبيّن لكم الخيط الأبيض
من الخيط الأسود من الفجر ثمّ أتموا الصّيام إلى الّليل
.
Na kuleni na kunyweni
mpaka ubainike kwenu weupe wa alfajiri katika weusi wa usiku . Kisha
timizeni saumu mpaka usiku .
Na katika sunna za funga
ya ramadhani ni kuchelewesha daku ili apate kuwa na nguvu wakati wa mchana
, na ni sunna vilevile kuharakiza kufutari ikiwa wakati umeshafika
,anasema Mtume s.a.w. :
لا تزال أمّتي بخير ما عجّلت الإفطار وأخّرت السحور .
Bado ingali umma wangu
watabaki katika kheri madhali wanafuturu mapema na wanachelewesha daku .
Na ni wajibu kuwa na
yakini wakati wa kufutari kwamba wakati umeshaingia kwa sababu asili ni
kubakia mchana na hairuhusuwi kula mpaka ithibiti kuingia kwa wakati wa
usiku . Na Haifai kufanya israfu katika vyakula na vinywaji wakati wa
kufutari , kwani Allah amekataza hayo katika kauli yake :
يا
بني آدم خذوا زينتكم عند كلّ مسجد وكلوا واشربوا ولا تسرفوا إنّه لا يحبّ
المسرفين .
Enyi wanaadamu! Chukueni
mapambo yenu (vaeni nguo zenu)wakati wa kila sala , na kuleni na kunyweni
vizuri . Lakini msipite kiasi tu , Hakika yeye Allah hawapendi wapitao
kiasi .
Na Amesema Allah:
إنّ المبذّرين كانوا إخوان
الشّياطين وكان الشّيطان لربّه كفورا .
Hakika watumiao kwa
ubadhirifu ni ndugu wa mashetani . Na shetani ni mwenye kumkufuru Mola
wake .
Kwa hivyo kuandaa kila
aina ya vyakula na vinywaji katika ramadhani na baadae kutupwa chakula
kilichobaki ni tabia inayokatazwa na sheria na hupoteza lile lengo hasa la
funga .
Na inashurutizwa kuwepo na
nia wakati wa kufunga imepokewa kutoka kwa Ibni Omar kutoka kwa ndugu yake
hafsa kwamba Mtume s.a.w. amesema :
من لم يبيّت الصّيام من الّليل فلا صيام له .
Asiyetia nia ya funga
tangu usiku basi huwa hana funga .
Basi mcheni Allah ndugu
waislamu na jitahidini kuitekeleza ibada hii tukufu kwa adabu zake na
sheria zake mtafaulu hapa duniani na kesho akhera .
والــســلام عـلـيـكـم ورحـمـة اللّه وبـركــاتــه
|