BARUA YA no: 2

Imeandikwa na: Rashid

                          Kutoka: Sultanate of Oman

Soma barua Iliyopita

BARUA HII IMESHASOMWA NA WATU: Hit Counter

 

MAMBO SITA YANAYOMWINGIZA MTU PEPONI.


Mtume S.A.W. ametumwa kwa binadamu na Majini ili awangoze katika njia ya haki itakayowatoa katika giza na kuwapeleka kwenye mwangaza wenye nuru kisha kufuzu na kuingia katika Pepo ya Mwenyezi Mungu S.W.T. ambayo upana wake ni sawa na mbingu na ardhi. Kwa hivyo Mtume S.A.W. ni Mtume wa umma huu uliosifiwa na Mola Mtukufu na pia ni Mwalimu wetu anayetuongoza katika mambo yote yanayohusu dini yetu ya Kiislamu. Lakini Mwislamu lazima afahamu kwamba amekalifishwa kutenda mambo mengi mema tuliyofunzwa na Mtume wetu ambaye hasemi neno lolote lile isipokuwa ni wahyi utokao kwa Mola wa walimwengu wote na ni maslaha kwa umma. Katika mambo hayo mema tumeahidiwa kwamba atakaetekeleza mambo sita basi bila shaka ataingia Peponi. Ingawa mambo hayo sita ni mepesi kuyasema kwa ulimi wakati mtu anaposoma kitabuni lakini kusema kweli ni magumu kuyatekeleza hasa kwa wakati huu tulionao. Kwani baadhi ya watu hivi sasa wanachukulia kwamba kusema uwongo kutamsaidia mtu kufanikisha lengo lake alilokusudia kama vile kupandishwa cheo chake kazini au kufitinisha watu au kuwapokonya watu mali yao. Na mara nyingi mtu anapoahidi mwishowe hushindwa kutekeleza hiyo ahadi.
Ukweli ulivyo hayo yote binadamu anayokimbilia kuyatenda kinyume na maamrisho ni kazi ya Shetani anayefanya bidii hiyo na kupandisha bendera yake katika kila kona ya ulimwengu huu kwa kuwapotosha watu kutenda yaliyoharamishwa kwa kuwapambia waja wa Mwenyezi Mungu Mtukufu kwamba wasiwe na wasiwasi wanayo fursa na umri mrefu wa kutubu, au hakuna lolote huko Akhera uhai ni wa hapa tu duniani mtu akifa ndio mwisho wa uhai wake. Siku hizi maasi mengi yameenea duniani kwa sababu watu wameacha dini yao na mila yao na kufuata mitindo ya makafiri kwa kudhani kwamba wao ndio watu walioendelea mbele kwa mavazi, maisha na mengi mengineo. Na ukweli huu unaonekana wazi na kila mmoja wetu, kwani siku hizi majina ya vitu vilivyoharamishwa yamegeuzwa kwa majina ya kupendeza kama vile: Zina imeitwa mahaba, ulevi ni kiburudisha-moyo, sigara kiondosha-mawazo na miziki ni utamaduni wa jadi. Na utaona watu waliowaiga hao makafiri hadi wamefikia wanaume kuvaa hereni, kusuka nywele na kurefusha nywele zao kama walivyo wanawake. Na haya yanawasababishia kusahau mipaka ya Mwenyezi Mungu S.W.T. na kujipa moyo ati ulimwengu wa sasa umebadilika na kuendelea mbele si kama ule wa zama za kale. Kwa hivyo mtu anakhiyari ya kufanya lolote lile analoona linampendeza. Jamani! Hebu tuzinduke na kasumba hii ya kuiga vitendo vya makafiri wanao upiga vita Uislamu na badala yake tuige Sunna na adabu za Mtume wetu alizofunzwa na Mola Mtukufu Mtume S.A.W. kasema:


"تكفلوا علي بست أتكفل لكم بالجنة. "قالوا: وما هي ؟ قال: "إذا حدث أحدكم فلا يكذب ، وإذا وعد فلا يخلف ، وإذا إئتمن فلا يخون ، وغضوا أبصاركم ، وكفوا أيديكم ، واحفظوا فروجكم".


Maana yake, “Nidhaminieni mambo sita nitakudhaminieni Pepo. Wakasema “Hayo ni yapi?” Akasema “Akizungumza mmoja wenu asiseme uwongo, na akiahidi asivunje miadi, na akiaminiwa asikhini, na inamisheni macho yenu (msitizame yaliyokatazwa), na zuieni mikono yenu (msiendee mambo ya haramu) na zihifadhini tupu zenu (msizini).”

Ndugu yenu: Rashid

Copyright © 2005  uislamu.net