|
|
HATARI YA
KUMSHABIHISHA ALLAH |
Shukurani
zote ni kwa Allah aliyeumba kila kitu, asiyekua na mwanzo wa kuwepo kwake,
na kila kitu ni kiumbe chake, hajafanana na kitu wala hakuna kitu
kilichofanana na yeye, na Rehma na Amani ziwe kwa Mtume wetu Muhammad (s.a.w)
aliyetumwa akiwa Rehma kwa Walimwengu wote, pamoja na Aali wake na Swahaba
wake na kila anayefuata uongofu wake mpaka siku ya Malipo (Amin).
Kumshabihisha Allah
mtukufu, ni kumfananisha yeye na mwengine asiyekua yeye, au mwengine
kumfananisha na Allah.
Kumshabihisha Allah
kunapatikana iwapo mtu ataitakidi kua Allah anasifika kwa sifa za Viumbe
wake, kama vile kuwa yeye ana Umbo, au Mkono au Mguu au Mdomo au Pua, au
kuwepo katika sehemu Fulani ikiwa ni Mbinguni au popote pale kama kukaa juu
ya Kiti, au kuitakidi kua Allah anaondoka kutoka sehemu moja kwenda sehemu
nyengine, au kuitakidi kua Allah ataonekana kwa Macho, na mengineo mfano wa
hayo.
Haya yote yamo katika
hukumu ya Kumshabihisha Allah.
HATARI YA KUMSHABIHISHA ALLAH MTUKUFU
Hakika kumshabihisha
Allah mtukufu ni hatari kubwa sana, na hatari hii inapatikana katika
kuitakidi mambo yaliyoko nje na uhakika wa Allah, kwa hivyo kunapelekea
katika upotevu, na mwisho wake ni kuporomosha utukufu wa Allah, na kuondosha
Heshima yake, na kuitakidi nje ya ukweli ulivyo.
Na kumshabihisha
Allah mtukufu ni mtihani walioupata wengi katika Umma zilizopita, hata
unaposoma yale yaliyorithiwa katika maandiko yao utayaona haya kwa uwazi
kabisa, zilifanya hayo kalamu za Waandishi, na Fikra za watu kwa kufuata
mapendwa Moyo yao na kuitika wasiwasi wa Kishetani, hata ikapelekea
kuitakidi kua Mungu yuko kama sisi katika Sura, Mfano na Namna, na kupelekea
kuchonga Masanamu ili iwe ni njia ya kumuabudia Allah aliyeumba.
Na sio ajabu kuona
Msiba wa kumshabihisha Allah kuwemo katika Umma huu vile vile katika baadhi
ya maandiko, na pengine hata kuyasikia hayo katika baadhi ya Mihadhara ya
Mashekhe, kwa hivyo tunapoyakuta tuwe macho tusije tukaingia katika Kosa
hilo kubwa.
Na hatari ya
Kumshabihisha Allah tunaweza kuileza katika haya yafuatayo:
1.
Kuondosha Upweke()
wa Allah.
Hili litapatikana ima
kwa kuliitakidi kwa kujua au bila ya kujua, kwa sababu unapompa Allah sifa
ya kumshabihisha tayari umeshaingia katika mlango wa kuitakidi kua Allah
hakuumba vitu vyote, kwa sababu haiwezekani kuwepo bila ya kupatikana yale
yaliyolazimika kupatikana katika kuwepo sifa ya kumshabihisha, kwa sababu
sifa yoyote ya Kiumbe ina mambo yanayolazimika kuwepo ili ipatikane Sifa
hiyo, kwa mfano Sehemu katika kupatikana Mkono au Mguu, kwa sababu vitu
hivyo haviwezi kupatikana mpaka ipatikane Sehemu ambayo ni ulazima wa
kupatikana kwake, Sasa unapoitakidi sifa ya kumshabihisha Allah tayari
umeshavunja Upweke wake, na kumfanya Allah kua ni mwenye uwezo katika Baadhi
ya Vitu tu, na kua yeye ameumba Baadhi ya Vitu tu, Ama vyengine kama Sehemu
itakua sio Kiumbe kwa sababu vilikua pamoja na yeye kwani Kuumba ni Kitendo
na Kitendo kinapatikana Baada ya Kuwepo Mtendeji. Allah atueke mbali na sifa
potofu za kumshabihisha.
2.
Kuondosha sifa ya Ukwasi().
Allah hahitaji kitu,
na sifa za viumbe ni zenye kuhitaji, kwa sababu zinahitaji Sehemu, wakati,
..; na vile vile mwenye sifa hizo anakua yumo katika kuzihitaji, kwa hivyo
unapoitakidi sifa ya Kumshabihisha Allah mtukufu tayari umeshaingia katika
Mlango huu wa kuitakidi kua Allah anahitaji, hakika Allah ametakasika na
kuhitaji.
3.
Kuitakidi Mabadiliko ya Allah.
Kwa kawaida Muislamu anaamini kua Allah ameumba kila kitu, na kua yeye ndiye
wa Mwanzo, na kila kitu kisichokua yeye ni kiumbe, kwa sababu yeye ameumba
kila kitu, na katika alivyoviumba ni vile vinavyolazimika kuwepo katika
kuviumba viumbe vyake, kama vile Sehemu, sasa unapoingia katika mtego wa
Kuitakidi sifa za kumshabihisha Allah, unajikuta tayari unamfanya Allah
katika Fikra zako kua ni kama kiumbe yumo katika yale waliyomo viumbe, kwa
hivyo ameshakua na sifa za kukubaliana na yale yanayokubaliana na viumbe,
kwa hivyo amebadilika kutoka katika Hali ya kwanza kabla hajaumba na kuingia
katika Hali ya pili katika kuumba na Baada ya kuumba, na hayo -sio
kuongezeka Sifa za Vitendo lakini- ni mabadiliko ya Dhati yake, na
kubadilika ni sifa iliyopatikana baada ya kukosekana, kwa hivyo Hali ya pili
ilikua Haipo, kutokana na Hayo itakua Allah ana mwanzo kama sisi viumbe, na
kuitakidi hivi ni Mizizi ya Ukafiri, Allah atuepushe nayo.
4.
Kujenga Sura ya Muumba katika Fikra ya mwenye kuitakidi.
Kwa hakika
unapoitakidi Sifa ya kumshabihisha Allah tayari unajenga Sura katika Fikra
yako, na kujenga Sura hiyo katika Kichwa ni Hatari kubwa sana, kwani tayari
umeshampa Umbile na umeshamfanya kua ni mwenye kuhitaji, na kumpa kila sifa
ambayo itamjaalia -katika fikra Zako- kua sawa sawa na Kiumbe, kwa hivyo
kunapelekea kuabudu Sura, jambo ambalo halina tofauti na kuabudu Sanamu.
Allah atuepushe na Fkra za Kishetani (Amin).
5.
Migongano na Waislamu.
Muislamu anapobeba
Itikadi potofu ya Kumashabihisha Allah, anakua tayari ni kama jeshi lenye
kubeba silaha ya kuwahujumu Waislamu, kwa sababu tayari ametofautiana nao
katika Msingi Mkuu wa Uislamu, nao ni Kumuamini Allah katika ukamilifu wa
Dhati yake na kua yeye hajafanana na chochote kile katika Viumbe vyake
Kidhati, wala hakuna kiumbe kilichofanana na yeye, lakini mwenye kuchukua
Itikadi hii sahihi -katika mtazamo wa mwenye kumshabihisha Allah- anakua
Bado hajamjua Allah, kutokana na hapo anaanza kumshambulia kua yeye ni
mwenye kuzipinga Sifa za Allah, na kua yeye Haabudu kitu, na kua yeye sio
Muislamu, kwani bado hajamkubali Allah kwa kumjua katika Sifa zake, na hapo
anakusudia zile Sifa za Kumshabihisha: Macho, Mikono, Miguu, Kuwepo katika
sehemu, Kukaa katika Kiti, Kuteremka kwa kuondoka Katika sehemu Moja na
kwenda katika Sehemu nyengine, kuonekana, n.k. Na mara nyengine utawaona
watu wenye itikadi hizi Wanawahukumu wale waliokhitalifiana nao kua sio
Waislamu, kwa hivyo hata kusali nyuma Yao Haifai. Allah atueke Mbali na kila
Fitna na kila Baya (Amin).
Ndugu yangu Muislamu
jihadhari usije ukawa ni Askari wa Shetani katika kuchukua Itikadi ya
Kumshabihisha Allah Mtukufu, na ukawa ni Sababu ya kuwatia Waislamu katika
Hukumu ya Ushirikina, na ujue kua haya tumeyaandika kama ni njia ya kuchuka
Hadhari kabla ya Kuja Athari, kwa sababu "Kinga ni Bora kuliko Tiba" kama
walivyosema.
Tunamuomba Allah
atueke mbali na fikra za Kumshabihisha na atueke Mbali na Fitna hiyo, na
atujaalie tuwe ni kitu kimoja (Amin).
Asante sana.
Ndugu yenu:
Hafidh.
H. Seif Sawafiy
Imam wa Msikiti wa Bujumbura (Burundi) |